Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Ofisi ya Rais - Ikulu

Mfuko wa Maendeleo ya Jamii

Habari

TASAF ilivyonufaisha walengwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Singida


Mnufaika wa Mpango wa TASAF Bi. Elizabeth Vicent akionesha Kondoo aliofanikiwa kuwamiliki baada ya kupokea ruzuku ya uzalishaji kupitia programu ya kukuza uchumi wa kaya.

Uhawilishaji wa Ruzuku ya Uzalishaji katika Halmashauri ya Wilaya ya Singida umefanikisha kuinua uchumi wa kaya za walengwa zilizokuwa na kipato duni.

Kaya hizo ambazo ziliingia kwenye Mpango wa TASAF  mwaka 2022, sasa zimeweza kumiliki mali  mbalimbali ikiwemo mifugo, kuboresha makazi sambamba na  kuwa na uwezo wa kumudu mahitaji mbalimbali ya kila siku.

Bi. Elizabeth Vicent, mkazi wa Kijiji cha Ifombou ni mmoja wa wanufaika wa TASAF  ambaye ameweza kumiliki kondoo, kuku, pamoja na  kuanza maandalizi ya kukarabati nyumba  kwa kununua bati 10 kupitia  ruzuku  ya msingi pamoja na  ruzuku ya uzalishaji  inayotolewa kupitia programu ya kukuza uchumi wa kaya.

Mnufaika huyu ambaye ni mama wa watoto watatu, anaeleza kwamba, tangu ameandikishwa kwenye Mpango na kuanza kupokea ruzuku, amekuwa akithaminiwa kwenye  jamii kutokana na kuwa na uwezo wa kuchangia mahitaji mbalimbali ya familia pamoja na kuwa na  shughuli ya kufanya.

“Huwa napokea shilingi 88,000 kama ruzuku kwa kipindi cha miezi miwili, fedha hiyo imekuwa inanisaidia kwenye mahitaji mbalimbali ambapo pia nimeweza kununua bati 10 kwa ajili ya nyumba, pia nilipokea ruzuku ya uzalishaji jumla ya shilingi 350,000 ambayo nilipokea kwa awamu mbili,” alieleza.

“Awamu ya kwanza nilipokea shilingi 175,000 ambayo nilitumia kununua kondoo watatu, na baadaye nikapokea shilingi 175,000 nyingine ambayo nayo nilinunua kondoo wawili na kufanya kuwa na jumla ya kondoo 5,” alisema.

Kwa kufuata miongozo na mafundisho ya ujasiliamali aliyopewa kabla ya kupokea ruzuku hiyo, Bi. Elizabeth aliweza kufanikiwa kuongeza kondoo wanne ambao walizaliwa kutokana na aliowanunua, pia amekuwa akiuza baadhi ya kuku wake ili kupata fedha za mahitaji madogo madogo wakati anasubiri fedha za ruzuku.

“Naishukuru Serikali na TASAF kwa kuleta  Mpango huu wa kutusaidia,  na sasa nimeweza kuwa na mali na pia nachangia kwenye  kipato cha kaya kwa kusaidia manunuzi ya mahitaji muhimu,” alisema.

Kwa upande wao, Bi. Mwanahamis Mugwu na Bi. Cecilia Samwa ambao pia ni wanufaika wa Mpango wa TASAF wamesema  kupitia Mpango huu wameweza  kujiunga kwenye vikundi vya kuweka akiba na kukopa hivyo kujiongezea  uwezo wa kuwa na fedha  ya matumizi na uwekezaji.