Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Ofisi ya Rais - Ikulu

Mfuko wa Maendeleo ya Jamii

Habari

Walengwa TASAF Hupatikana kwa Uwazi - Ridhiwani Kikwete


Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete amesema mchakato wa kuwapata walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini (TASAF) hupatikana kupitia mkutano wa  wananchi  wa eneo husika na mchakato hufanyika kwa uwazi pasipo na upendeleo. Mhe. Ridhiwani ameyasema hayo mbele ya Kamati ya Bunge ya  Utawala, Katiba na Sheria katika kikao cha kupokea  taarifa ya utendaji  wa  Mfuko wa  Maendeleo ya Jamii  kwa kipindi cha  Mwezi Machi  hadi Juni 2023. Alitoa ufafanuzi huo wakati akijibu hoja za wajumbe wa kamati hiyo Mhe. Abdullah Ali Mwinyi, Mhe Agnesta Lambert na Mhe. Tumaini Magessa ambao waliuliza kuhusuana na vigezo vya kuwapata walengwa pamoja na miradi mbalimbali inayotekelezwa na TASAF.

Alisema kuna utaratibu mahususi ambao unatumika  katika kuwapata walengwa na wanufaika,  unaanzia katika ngazi ya kijiji na mtaa, ambapo Mwenyekiti wa kijiji  au mtaa huitisha kikao cha wananchi ambao ndio hupendekeza vigezo vya kaya maskini na baadae majina ya watu wenye hali  duni  kiuchumi ili waingie kwenye mpango. “Na utaratibu wa kuwapata  walengwa huwa ni wa uwazi  na shirikishi kwa watu wote, na wale ambao  majina yao yamependekezwa ili waingie kwenye mpango na wale wanaotolewa kwa kutokukidhi vigezo  vilivyowekwa, huwa wanapewa fursa ya kukata rufaa pale ambapo wanakuwa hawajaridhika na hatua  zilizochukuliwa”, alisema Naibu waziri.

Pia, Mhe. Ridhiwani alisema wanufaika wa TASAF wanapiga hatua kila siku, akisema hadi sasa wapo walengwa wengi waliofanya vizuri kupitia mapango huu. Aliongeza kuwa hadi sasa kuna kaya 78,895 ambazo zimekidhi vigezo vya kutoka katika mpango wa TASAF, lakini wengi wao hawapo tayari kutolewa kwa hofu kuwa hawataweza kujitegemea wakiwa nje ya Mpango.

“Changamoto iliyopo ni kwamba watu wanaweza kujitokeza mbele ya hadhara kuelezea mafanikio, lakini wakiambiwa watoke nje ya mfumo ili kuwapisha wengine, hawakubali. Hili lipo maeneo mengi, tunaendelea kutoa elimu ya ujasiriamali waweze kujitegemea”, alisema Naibu Waziri. Hata hivyo, Mhe. Kikwete alisema hivi sasa Serikali inafanya tathimini ya hali za walengwa katika Maeneo 72 ya Utekelezaji.

Akizungumzia kuhusu Miradi ya Jamii, Mhe. Ridhiwani alisema miradi hiyo hubuniwa na wananchi  wa eneo husika kulingana na changamoto wanayokutana nayo na kwamba utekelezwaji wake hutegemea nguvu kazi  kutoka katika kaya za walengwa  ambao  hulipwa ujira kwa kazi hiyo. “Hii ni miradi ambayo hutumika kuzalisha ajira za muda kwa walengwa, na miradi hii hubuniwa na wananchi wa eneo husika, pale inapooneka kuna changamoto katika utelekezwaji wake, basi walengwa huruhusiwa kubadili aina ya mradi”, alisema wakati anajibu swali la Mhe. Tumaini Magessa mbuge wa jimbo la Busanda aliyetaka kujua kwa nini walengwa hufanyishwa kazi.

Kwa upande wake Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. George Simbachawene alisema Serikali imekuwa ikichukua hatua za kuwaondoa kwenye mpango wanufaika wote walioingizwa kwenye mpango pasipo kukidhi sifa zilizowekwa. “Serikali imekuwa ikitoa maelekezo ya mara kwa mara ikisisitiza wanaostahili ni walengwa na kuondolewa walioingizwa pasipokuwa na sifa. Kigezo chetu ni kuchukua wananchi wenye hali ya chini ili kuwasaidia, changamoto inakuja kwenye namna ya kuwapata, lakini tunaendelea kuboresha eneo hili”, alisema Mhe. Simbachawene.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa kamati hiyo, Mhe. Dkt. Joseph Mhagama  aliipongeza Serikali na TASAF kwa   kazi nzuri  inayofanyika  ya kuratibu na kuendelea na miradi  mbalimbali  ya  kunusuru kaya masikini. Mhe. Dkt Mhagama alishauri TASAF kuhakikisha miradi yote ya jamii inayotekelezwa katika maeneo mbalimbali nchini inakuwa na ubora ili idumu kwa muda mrefu na kuangalia uwezekano wa kuwafanya wanufailka wa miradi hii wawe sehemu ya umiliki baada ya kukamilika kwake. “Tumeona shughuli mbalimbali ambazo zinafanyika kupitia TASAF katika kuinua na kuimarisha vipato vya kaya maskini, juhudi hizi ni nzuri na tunapendekeza kuendelea na maboresho mbalimbali katika maeneo muhimu ili kuleta tija zaidi”, alisema Mhe. Mhagama.