Habari
Waziri ataka walioboresha maisha wajitoe TASAF

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Jenista Mhagama amewataka wanufaika wa Mpango wa Kunusuru Kaya za Walengwa ambao uchumi wa kaya zao umeimarika wajiondoe kwa hiyari ili kuwapa nafasi wengine.
Waziri Mhagama ambaye ofisi yake inaratibu Mfuko wa Maendeleo ya Jamii - TASAF ameyasema hayo Jumamosi Juni 4 2022 katika kijiji cha Ilongero mkoani Singida alipokuwa akizungumza na wananchi wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Serikali za Mitaa na Utawala Bora.
Awali, Ofisa Mtendaji wa kijiji hicho, Josephine Komba alieleza kuwa baadhi ya walengwa waliofanikiwa huogopa kusema mafanikio yao kwa kuhofia kuondolewa kwenye mpango. Hata hivyo wanaufaika wawili wa Mpango, Pili Mohammed anayefanya biashara ya mbogamboga sokoni na Tatu Sima wameeleza jinsi walivyonufaika na Mpango ambao umefanya kazi kubwa ya kuwaondoa wananchi wengi katika umasikini na kuingia hali nzuri zaidi.
Wanufaika katika kijiji cha Ilongero chenye walengwa 278 wameshiriki kuchimba malambo mawili katika vitongoji vya Mitunduruni na Mkese na kutatua tatizo la maji.